Wito umetolewa kwa wakenya kudumisha Amani hasa taifa linapoelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka 2022.
Akizungumza wakati wa hafla ya ufunguzi wa kanisa la mtakatifu Mariko katika eneo bunge la Kapseret, Gavana wa Kaunti ya Uasin Gishu Jackson Mandago aidha amewataka wakenya kujiepusha na siasa za chuki na ukabila.
Mandago vile vile ameliomba kanisa kuwa kipao mbele kwa kuombea taifa na kuhubiri Amani huku akiwakashifu wanasiasa wanaoneza siasa za chuki, ubaguzi na ukabila.

“Mahali tumetoka na tunapoelekea, tunaelewa kama kaunti msingi wa maendeleo ni amani dhabiti tuliyonayo nayo kwa sasa, na hatuezi kamwe kurudi nyuma. Nawapongeza wananchi wa kaunti hii, tumeheshimika sana sehemu nyingi za Kenya kwa sababu sisi tumewaruhusu wanasiasa wengine waje waombe kura, na hatujakuwa na rabsha wala vurugu mpaka sasa. Lo kila mahali wanasema fanyeni siasa kama Uasin Gishu na kwa hivyo tuendelee vivyo hivyo.”
– Gavana Mandago.
Uasin Gishu aliathirika pakubwa na vurugu za baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2007 zilizoplekea vifo vya zaidi ya wakenya 1,000 na mamia yaw engine kufurushwa makwao.
Baadaye Mandago alijumuika na waumini kwa sherehe ya Padri Jonas Kiplimo akiadhimisha miaka kumi ya upadri katika Kaunti ya Elgeyo Marakwet.

Aidha alihudhuria harambee ya kuchangisha fedha za matibabu ya Mzee David Koech kwenye wadi ya Tembelio, eneo bunge la Moiben.